Home » » PINDA AIONYA CCM UTEUZI WA WAGOMBEA

PINDA AIONYA CCM UTEUZI WA WAGOMBEA

Waziri Mkuu Mizengo Pinda amezitaka ngazi mbalimbali za uteuzi wa wagombea wa CCM kuwapa wananchi nafasi kuchagua watu wanaowataka ili kuepuka kupoteza viti katika uchaguzi.
Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo juzi jioni wakati akiwahutubia maelfu ya wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Mikutano wa Kashaulili, Mpanda mkoani hapa.
Pia alitumia mkutano huo kuaga jimboni humo akisema muda wa kuendelea kuwa Mbunge wa Katavi umetosha na sasa anatafuta kitu kingine cha kufanya.
Kwa mara ya kwanza, Pinda alichaguliwa kuwa Mbunge wa Mpanda Mashariki (sasa Katavi) mwaka 2000 na ameongoza jimbo hilo kwa mihula mitatu.
Kuhusu uteuzi
Akizungumzia uteuzi wa wagombea mbalimbali, Pinda aliwaasa viongozi wa CCM kuwateua watu wanaofaa kugombea uongozi kwenye nafasi mbalimbali wale ambao wanakubalika na wananchi na wawape nafasi wananchi kuchagua mtu wanayemtaka.
Alisema haifai CCM kuwalazimisha kwa kuwachagulia wananchi kiongozi wasiyemtaka... “Kumekuwa na tabia ya kuteua watu ambao hawakubaliki kwa wananchi na matokeo yake watu hao wamekuwa wakishindwa kwenye uchaguzi... acheni chuki, msiteue watu kuwania uongozi kwa ajili ya kupewa pesa na urafiki,” alisema.
Pinda aliyetangaza ni ya kuwania urais kimyakimya, aliwataka Watanzania kutowachagua watu wanaotaka kiti hicho na vile vya ubunge na udiwani kwa kutanguliza fedha.
“Watu hao wanaotafuta uongozi kwa kutoa rushwa kwa wananchi ni hatari, kuweni makini kwa kuchagua viongozi waadilifu watakaoongoza kwa kutanguliza mbele utaifa kuliko masilahi yao binafsi.
“Wako watu wanaotaka uongozi kwa kuhonga wapigakura, watu wa namna hiyo hawafai kuwa wagombea wa urais, ubunge na udiwani kwa kuwa si waadilifu na wakishapata uongozi kamwe hawezi kuwajali wananchi kwanza watataka kurudisha fedha walizotoa.
“Hakikisheni mnachagua viongozi ambao wanaweza kuwaongoza kwenye maeneo yenu na siyo vinginevyo, achaneni na watu wanaowapa pesa hao hawatawapeleka kokote badala yake watakuwa viongozi wabinafsi kwa kutanguliza masilahi yao mbele na kuwasahau wananchi waliowaweka madarakani,” alisema Pinda.
Alisema: “Watu wanaotaka uongozi kwa fedha, wanapowaletea hizo pesa kuleni lakini mhakikishe wakati wa uchaguzi hamwapigii kura.”
Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Katavi yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa