Home » » WADAU wa maendeleo mkoani Rukwa wametakiwa kuchangamkia fursa za uwekezaji hususani katika sekta ya Elimu

WADAU wa maendeleo mkoani Rukwa wametakiwa kuchangamkia fursa za uwekezaji hususani katika sekta ya Elimu

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
WADAU wa maendeleo mkoani Rukwa wametakiwa kuchangamkia fursa za uwekezaji hususani katika sekta ya elimu ili iwe chachu ya kuongeza wataalamu wa kada mbalimbali mkoani humo ambao watasaidia kupatikana kwa maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii.

Ushauri huo umetolewa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya CCM mkoani  Rukwa, Rainer Lukara wakata akizungumza kwenye uzinduzi wa sherehe za wiki ya wazazi mkoani humo zilizofanyika kwenye kijiji cha Malongwe na Swaila kwenye kata ya Mkwamba wilayani Nkasi mkoani humo.

Akisoma taarifa ya Mwenyekiti huyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Clement Bakuli alisema kuwa Rukwa ni moja ya mikoa michache nchini ambayo ina fursa nyingi za uwekezaji katika nyanja mbalimbali zikiwemo za kielimu ambazo hazijatumika ipasavyo na zinahitaji uwekezaji wenye tija hivyo wananchi wanapaswa kuwakaribisha wawekezaji kwenye sekta hiyo.

"Elimu ndio chachu ya mafanikio ya kila kitu hivyo sasa lazima tukubali kukaribisha wawekezaji kwenye eneo hilo ili watusaidie kuwekeza kwa kujenga, shule za msingi na za sekondari sambamba na vyuo vya kutoa elimu ya juu vyenye kutoa elimu yenye kuleta tija kwa vijana wetu......kupitia uwekezaji huo ndio tutapata wataalamu mbalimbali wakiwemo wa idara ya afya, elimu na wengineo ambao kwa sasa tunawapata kwa shida kutokana na wengi wao kukataa kufanya kazi katika mkoa wetu" alisema

Aliongeza kuwa pamoja na kuwepo kwa jitihada kadhaa za kuwashawishi watumishi wa kada hizo, ikiwemo ya kuwepo kwa mfuko wa kumotisha watumishi ili wakubali kwenda Rukwa kufanya kazi lakini wamekuwa wakigoma hata wanaokubali  kukaa kwa kipindi kifupi kisha ulazimika kuondoka kwa madai ya mazingira magumu ya kazi.

 "tusiwe na fikra potofu za kuogopa na kukataa uwekezaji kwani hatutapata maendeleo yoyote ya kwetu binafsi wala ya mkoa.......... tuwakaribishe na tuingie nao ubia, naamini kwa kuwa wenzetu wanakuwa wamejiandaa vizuri kiuchumi utaona kasi ya maendeleo itakavyokuwa kubwa ukilinganisha na sasa hivi" alisema Lukara ambaye pia ni mfanyabiashara maarufu mjini hapa.

Mkoa wa Rukwa ni moja ya mikoa katika ukanda wa ziwa Tanganyika ambayo imetangaza vivutio vya uwekezaji katika nyanja mbalimbali ikiwemo ya elimu ambapo hasa bado kasi ya uwekezaji kwenye elimu si ya kuridhisha kwani mkoa huo una shule za msingi 357  na za sekondari 89 pekee kitu ambacho bado kinaonyesha kuhitaji wawekezaji kwenye eneo hilo.

Awali, akisoma risala kwenye sherehe hizo mkazi wa kijiji hicho Isack Lyande alisema kuwa shule ya msingi kwenye kijiji hicho inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya kukosa madarasa matatu hivyo kusababisha wanafunzi wengine kusomea chini ya miti.

Alitaka serikali kuliangalia suala hilo na kuona namna ya kulitafutia ufumbuzi wa kudumu kwani chachu ya kuathiri maendeleo ya kitaaluma ya mwanafunzi na imekuwa ikiwakatisha tamaa na walimu kutoa elimu yenye ubora.
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Katavi yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa