Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MAMA na mtoto wake, wakazi wa Kijiji cha Mnyagala, Tarafa ya
Kabungu, Wilaya ya Mpanda, mkoani Katavi, wamefariki dunia baada ya
kupigwa na radi wakiwa njiani kuelekea nyumbani kwao.
Waliokufa wametajwa kuwa ni Migu Samwel (46) na mwanae Nsungulwa Kasanzu (15).
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari, alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 12 jioni kijijini hapo.
Alisema kabla ya vifo hivyo mama huyo na mwanae walikuwa wamekwenda
kwa jirani yao kumsalimia na walipoona dalili za mvua waliaga kabla
mvua haijaanza kunyesha.
Alisema walipofika jirani na nyumba yao umbali wa mita 15 ndipo
walipopigwa na radi na kufariki dunia papo hapo. Mama alipigwa na
radi sehemu ya kifuani na mwanae alipigwa na radi sehemu ya
kichwani.
Miili ya marehemu hao ilitarajiwa kuzikwa jana kijijini hapo baada ya taratibu za kidaktari kukamilika.
Wakati huohuo, Paulina David (3), mkazi wa Kijiji cha
Sungamila, Kata ya Kasokola, Wilaya ya Mlele, amefariki dunia
baada ya kutumbukia ndani ya ndoo ya maji akiwa nyumbani kwao.
Tukio hilo lilitokea juzi saa 10 jioni wakati mtoto huyo alipokuwa akicheza na dada yake, Stella David (5).
Wakati tukio hilo linatokea mama wa watoto hao alikuwa amekwenda mtoni kufua nguo
Chanzo:Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment