Home » » Wachina wampa Pinda pikipiki 44

Wachina wampa Pinda pikipiki 44

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amepokea msaada wa pikipiki 44  kutoka Ubalozi wa China na Kampuni ya Fu-Tang  ya nchini humo.
 
 Msaada huo alikabidhiwa juzi mbele ya viongozi wa Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi katika hafla fupi iliyofanyika Kijiji cha Kibaoni.
 
Akizungumza na viongozi wa wilaya hiyo pamoja na wakazi wa kijiji hicho kabla ya kukabidhi msaada huo, Balozi wa China nchini, Dk. Lu Youqing, alisema anaamini kupatikana kwa pikipiki hizo kutasaidia kuleta maendeleo ya haraka ya wilaya hiyo.
 
“Tunataraji matumizi ya pikipiki hizi yatasaidia kuleta maendeleo ya haraka na hatimaye kuongeza kipato cha wakazi wa wilaya hii,” alisema Balozi Lu ambaye ofisi yake imekabidhi pikipiki 20.
 
Alisema raia wa nchi yake wanafikia bilioni 1.3 na yeye anatamani kuona walau kila mmoja akinunua walau kilo moja ya chakula kutoka Tanzania  ili waweze kuongeza soko kwa mazao yanayozalishwa na wakulima wa Tanzania.
 
Naye Meneja Mkuu wa kiwanda cha kutengeneza pikipiki cha FEKON ambayo ni kampuni tanzu ya Fu-Tang,  Zheng Bing, alisema taratibu zitakapokamilika, wana lengo la kujenga kiwanda cha kutengeneza pikipiki na kompyuta ili kuongeza ajira kwa Watanzania. Kampuni hiyo ilikabidhi pikipiki 24.
 
Akipokea msaada huo, Waziri Mkuu alimshukuru Balozi Lu   na kampuni ya Futang na kuahidi kuzigawa ili ziwasaidie watendaji kusimamia kazi  hivyo kuharakisha kuleta maendeleo kwa wakazi wa wilaya hiyo.
 
" Tuna kata 24  kwenye wilaya yetu kwa hiyo kila kata itapewa pikipiki moja. Hiyo pikipiki siyo ya Katibu Kata binafsi bali ni ya kata, kwa hiyo Katibu Kata atakuwa ndiyo msimamizi,” alisema Pinda ambaye . yuko kijijini kwake Kibaoni kwa mapumziko ya mwisho wa mwaka.
 
Alisema  pikipiki saba zitapelekwa kwenye vituo vitano vya afya vya Mamba, Usevya, Inyonga, Katumba na Kanoge na zahanati za Nsimbo na Kasansa.
 
“Pia tutapeleka pikipiki nyingine nane katika shule za sekondari za Sitalike, Machimboni, Magamba, Nsimbo na Mtapenda. Nyingine ni Utende, Inyonga na Kasokola,”  aliongeza.
 
Wengine watakaofadika na mgao huo ni watendaji wa Chama Cha Mapinduzi  (CCM) wa Wilaya hiyo kwa kila mmoja kupatiwa moja, jumuiya za chama  tatu na moja iliyobakia itagawiwa kwa CCM Mkoa wa Katavi.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Katavi yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa