Home » » Nsimbo yapiga marufuku usambazaji mbegu za mahindi

Nsimbo yapiga marufuku usambazaji mbegu za mahindi

BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Nsimbo, Wilaya ya Mlele, Katavi, limepiga marufuku ugawaji wa mbegu zinazotolewa kwa vocha za ruzuku aina ya PANA 4 M 19 katika halmashauri hiyo kutokana na mbegu hizo kutokuwa na ubora.
Uamuzi huo ulitolewa hapo juzi kwenye kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Nsimbo.
Madiwani wa halmashauri hiyo walitoa malalamiko ya mbegu hizo kutokuwa na ubora na kufanya zishindwe kuota na kuwasababishia wakulima hasara.
Diwani wa kwanza kutoa malalamiko alikuwa ni Diwani wa Kapalala, Rewards Sichone, aliyeeleza kwamba wakulima wa kata yake walichukua mbegu za mahindi aina ya Pana zinazotengezwa mkoani Arusha ambazo zimeshindwa kuota kutokana na kukosa ubora.
Alieleza pia mawakala wa pembejeo wamekuwa wakiwauzia wakulima pembejeo bila kubandika bei kwenye maduka yao na matokeo yake wamekuwa wakiuza bei kubwa kuliko iliyopangwa na serikali.
Sichone alitoa mfano wa bei ya mbolea  aina ya UREA ambayo wakala badala ya kuuza kwa sh 20,500 yeye anauza sh 26,500 na kwamba baada ya kugundua alimfuata wakala huyo na kumtaka awarudishie kiwango cha fedha alichowazidishia. Tayari wakala huyo ameanza kurudisha fedha hizo kwa wakulima.
Diwani wa Magamba, Philip Kalyalya, alieleza tatizo la mbegu kutoota lipo  pia kwenye kata yake, hivyo aliomba wakulima waliopanda mbegu hizo na kushindwa kuota walipwe fidia na wakala anyang’anywe vocha zote za ruzuku  ili asilipwe fedha na serikali.
Diwani wa Kasokola, Crisanti  Mwanawima  alishauri  kabla ya mbegu kusambazwa kwa wakulima ziwe zinakaguliwa na wataalamu wa kilimo  ili kukabiliana na tatizo kama hilo.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Nsimbo, Mohamed Assenga, alitaka  Ofisa Kilimo wa halmashauri hiyo,  Rodrick Ntulo, kueleza baraza hilo sababu za mbegu hizo kushindwa kuota.
Ntulo alikiri kupokea kwa taarifa za mbegu hizo kutoka kata mbalimbali na ndipo idara hiyo ya kilimo kupitia wataalamu wake walipoamua kuzifanyia majaribio na kubaini hazikuweza  kuota.
Alisema kutokana na hali hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Mlele ameishaanza  kuchukua hatua kwa kuwaandikia barua wakala mkuu wa pembejeo akimtaka asisambaze na kugawa mbegu hizo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Katavi yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa